Lowassa: Kuna dalili za 'udikteta' serikalini Tanzania

Kiongozi wa upinzani nchini Tanzania Edward Lowassa amemkosoa mpinzani wake rais John Magufuli kwa kile alichokitaja kuwa ''chembechembe za kidikteta'' nchini humo.
Akizungumza na mwandishi wa BBC John Nene nchini Kenya, amesema kuwa alitaraji kwamba rais Magufuli angeondoa urasimu serikalini lakini "kuna mambo mengine hayajakwenda sawa ", ijapokuwa alikataa kutoa mifano alipotakiwa kufanya hivyo.
Bwana Lowassa alikuwa katika chama tawala alipokuwa waziri mkuu, lakini mwaka uliopita alijiunga na upinzani wa CHADEMA ambapo alishindwa na Rais Magufuli wakati wa uchaguzi.
Magufuli aliyepewa jina Tinga (Bulldozer) anajulikana kufanya maamuzi yanayopendwa tangu achukue mamlaka mwaka uliopita, kama vile kufutilia mbali sherehe za uhuru wa taifa hilo ili kuhifadhi fedha.
Lakini wakosoaji wake wamemshtumu kwa kukabiliana vikali na wapinzani.
Gazeti moja linalodaiwa kuwa mkosoaji mkubwa wa uongozi wake hivi majuzi lilifungwa huku mtu mmoja akikamatwa kwa madai ya kumtusi katika mitandao ya kijamii.
Serikali yake pia imepiga marufuku mikutano ya hadhara pamoja ile ya faraghani ya kisiasa.
Maandamano ya upinzani yaliyopangwa kufanywa dhidi ya serikali yaliahirishwa mwezi huu baada ya viongozi wa kidini kujitolea kuongoza mazungumzo na serikali.
Bwana Lowassa amesema kuwa maandamano yalilenga kupinga ''chembechembe za udikteta katika serikali'.
Aliambia wanahabari kwamba ana matumaini kuhusu mazungumzo hayo lakini hatosema kile upinzani utakachofanya iwapo yatafeli.

Post a Comment

0 Comments